Wiki ya Utumishi wa Umma 2025 - TIRA Tunashiriki

Mei 28,2025, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw.Juma Mkomi alizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu maadhimisho ya siku ya Utumishi wa Umma, mwaka 2025, ambapo aliwakaribisha wananchi kuhudhuria maonesho hayo katika viwanja vya Chinangali Park kuanzia Juni 16-23 , 2025 ambapo huduma mbalimbali zitatolewa.
Katibu Mkuu alieleza katika maadhimisho ya mwaka huu, Wizara, Sekretarieti za Mikoa na Taasisi za Umma zitafanya maonesho na kutoa elimu kuhusu utekelezaji wa majukumu ya taasisi zao katika Viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma kuanzia tarehe 16-23 Juni, 2025. Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania tutashiriki kutoa elimu kuhusu utekelezaji wa majukumu yetu katika sekta ya bima.
Bw. Mkomi pia alieleza siku ya Utumishi wa Umma Barani Afrika ni siku maalum ya Watumishi wa Umma ambayo husherehekewa tarehe 23 Juni kila mwaka na Nchi wanachama wa Umoja wa Afrika (AU) kwa lengo la kutambua mchango wa Watumishi wa Umma katika maendeleo ya Nchi zao na Bara la Afrika kwa ujumla.
Pia alieleza Chimbuko la Sherehe hizi ni uamuzi wa Mkutano wa Mawaziri wenye dhamana ya Utumishi wa Umma uliofanyika Tangiers Nchini Morocco mwaka 1994 na uamuzi huo ulizitaka Nchi za Afrika kusherehekea siku hii kwa kauli mbiu moja katika Bara zima la Afrika.