Mjadala wa Bima watoa jukwaa la elimu na ushindani kwa vijana
Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), imeshiriki mjadala mkubwa wa masuala ya Bima ulioandaliwa na Taasisi ya Bima Tanzania (IIT) kwa lengo la kuongeza uelewa wa masuala ya Bima kwa vijana pamoja na kupima ujuzi wao kuhusu sekta hiyo.
Mjadala huo uliofanyika Mei 16, 2026 uliwakutanisha wanafunzi kutoka shule mbalimbali za sekondari, vyuo vikuu pamoja na wadau wa sekta ya Bima nchini Tanzania ambapo mada mbalimbali zilijadiliwa ikiwemo umuhimu wa wazazi kuwashirikisha watoto katika masuala ya Bima, nafasi ya Bima ndogo katika jamii pamoja na hoja kuhusu iwapo Bima ni anasa au hitaji muhimu kwa maisha ya kila siku.
Katika mashindano hayo, shule ya sekondari ya Shabaan Robert iliibuka mshindi kwa upande wa shule za sekondari baada ya kufanya vizuri katika mijadala hiyo, huku Chuo kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM) kimeibuka mshindi kwa upande wa vyuo vikuu.
TIRA ilishiriki kama msimamizi mkuu wa sekta ya Bima nchini ambapo Meneja wa TIRA Kanda ya Mashariki, Bw. Zakaria Muyengi, alikuwa Jaji Mkuu wa mjadala huo.
Akizungumza katika mjadala huo pamoja na wadau wengine amesisitiza umuhimu wa kuwajengea vijana uelewa wa mapema kuhusu Bima ili waweze kufanya maamuzi sahihi ya kifedha na kujenga utamaduni wa kujikinga dhidi ya majanga na hatari mbalimbali katika maisha yao.
Miongoni mwa shule na vyuo vilivyoshiriki mjadala huo ni Kisutu Sekondari, Zanaki Sekondari, Jangwani Sekondari, Shabaan Robert Sekondari, Tambaza Sekondari, Theodora Sekondari, Chuo Cha Ardhi, Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam na Chuo Cha Uhasibu Arusha.
Mjadala huo umeelezwa kuwa sehemu ya juhudi za kuendelea kutoa elimu ya Bima kwa jamii, hususan kwa vijana ambao ni nguvu kazi na viongozi wa baadaye wa taifa.
