Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania

TIRA Logo
TIRA NA NHIF zajadili mpango wa utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote
18 May, 2026
TIRA NA NHIF zajadili mpango wa utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote

Kamishna wa Bima wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania, Dkt. Baghayo Saqware, leo Mei 18, 2026 amekutana na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Dkt. Irene C. Isaka, na kujadili masuala mbalimbali yanayohusu utekelezaji na usimamizi wa Bima ya Afya kwa Wote nchini.

 

Mazungumzo hayo yalitanguliwa na wasilisho la andiko kuhusu uhalali na umuhimu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kushiriki kikamilifu katika kuwezesha jukumu la TIRA la usimamizi wa sekta ya bima nchini.

Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Baghayo Saqware amesema kuwa Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) inaendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma ya Bima ya Afya ifikapo mwaka 2030. Aidha, amesema mamlaka hiyo inathamini ushirikiano unaoendelea kati ya TIRA, Wizara ya Afya pamoja na wadau wengine, na itaendelea kutoa mchango wa kitaalamu na kiufundi katika kufanikisha utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote.

Kwa upande wake, Dkt. Irene C. Isaka ameishukuru Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania kwa ushirikiano mkubwa unaoendelea kuimarisha utendaji kazi wa taasisi hizo mbili. Pia ameahidi kuendeleza ushirikiano huo muhimu ili kuhakikisha utekelezaji thabiti na usimamizi madhubuti wa Bima ya Afya kwa Wote nchini.