Wananchi Kigoma Waelimishwa kuhusu Bima na Fursa zake
Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) kupitia Kanda ya Ziwa Tanganyika inashiriki katika Maonesho ya Lake Tanganyika International Expo 2026 yanayofanyika katika Viwanja vya Mwanga Community City, Kigoma kuanzia tarehe 16 – 22 Septemba 2026. Ushiriki huo unalenga kutoa elimu kwa umma kuhusu masuala mbalimbali ya bima, ikiwemo umuhimu wa kuwa na bima, aina za bima zinazopatikana pamoja na haki na wajibu wa watumiaji wa huduma za bima.

Aidha, wananchi wanaelimishwa kuhusu fursa zilizopo katika sekta ya bima, ikiwemo fursa ya kuanzisha biashara zinazohusiana na huduma za bima kama kufanya shughuli za uwakala wa bima. Elimu hiyo imekuwa na mwitikio chanya kutoka kwa wananchi, ambapo wengi wameonesha hamu ya kujua zaidi kuhusu taratibu, mahitaji na fursa zinazopatikana katika kufanya shughuli za uwakala na biashara za bima.

Maonesho hayo yanatoa fursa kwa TIRA kukutana na wananchi na wadau mbalimbali na kuwawezesha kupata uelewa mpana kuhusu huduma za bima, huku wananchi wakipata nafasi ya kuuliza maswali na kupata ufafanuzi wa moja kwa moja kutoka kwa wataalamu wa bima.

Uzinduzi rasmi wa Maonesho hayo unatarajiwa kufanyika kesho, tarehe 18 Septemba 2026, katika Viwanja vya Mwanga Community City, Kigoma. Mgeni Rasmi katika uzinduzi huo anatarajiwa kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga.
TIRA, Kwa Soko Salama la Bima
