Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania

TIRA Logo
Vitambulisho vya bima ya afya kwa wenye mahitaji maalum vyazinduliwa Tabora
28 Feb, 2026
Vitambulisho vya bima ya afya kwa wenye mahitaji maalum vyazinduliwa Tabora

Tarehe 27 Februari 2026, Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) Kanda ya Magharibi – Tabora imeshiriki katika uzinduzi wa awamu ya kwanza ya mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, sambamba na zoezi la ugawaji wa kadi kwa makundi maalum. Hafla hiyo imefanyika katika Viwanja vya Stendi ya Zamani, Nzega, na kuhudhuriwa na viongozi wa Serikali, wadau wa sekta ya afya pamoja na wananchi wa Wilaya ya Nzega.

Akihutubia katika hafla hiyo, Mgeni Rasmi Mhe. Naitapwaki Tukai, Mkuu wa Wilaya ya Nzega, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora, alisema: “Uzinduzi huu ni sehemu ya jitihada za Serikali kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma za afya bila vikwazo vya kifedha.” Kupitia mpango huo, wananchi wanatarajiwa kunufaika na huduma bora za afya kwa gharama nafuu na kwa wakati.

Kwa upande wake, mwakilishi wa TIRA Kanda ya Magharibi, Bi. Awanje Matenda, alisema TIRA itaendelea kusimamia na kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa kuwa na bima ya afya ili kuongeza uelewa na ushiriki wa wananchi katika mifumo rasmi ya bima. Alisisitiza kuwa bima ni kinga muhimu dhidi ya gharama kubwa za matibabu zisizotarajiwa.

Katika zoezi hilo, makundi maalum wakiwemo wazee, watu wenye mahitaji maalum na wananchi wenye kipato cha chini walikabidhiwa kadi zao za bima ya afya, hatua itakayowawezesha kuanza kunufaika mara moja na huduma za matibabu katika vituo vilivyosajiliwa.

TIRA Kanda ya Magharibi imeahidi kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhamasisha jamii kujiunga na Bima ya Afya kwa Wote, kwa lengo la kufikia azma ya Serikali ya kuwa na jamii yenye afya bora na ustawi endelevu.