The United Republic of Tanzania

Tanzania Insurance Regulatory Authority

“TIRA kwa Soko Salama la Bima”
TIRA yatunukiwa Tuzo ya Shukrani kwa Mchango katika Nishati Safi ya Kupikia
12 Aug, 2026
TIRA yatunukiwa Tuzo ya Shukrani kwa Mchango katika Nishati Safi ya Kupikia

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imetunukiwa Tuzo ya Shukrani na Mwanamke Initiatives Foundation kwa kutambua mchango na ushirikiano wake katika kufanikisha Mdahalo wa Nishati Safi ya Kupikia uliofanyika katika Hoteli ya Kwanza, Kizimkazi, Zanzibar.

Tuzo hiyo ilikabidhiwa tarehe 11 Agosti 2026 katika hafla iliyohudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye alikuwa Mgeni Rasmi, pamoja na viongozi mbalimbali wa Serikali, viongozi wastaafu, viongozi wa dini, wafanyabiashara na wachimbaji wa madini nchini.

Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amepongeza juhudi zinazofanywa na wadau mbalimbali wa maendeleo katika kuwawezesha vijana, akitolea mfano Mwanamke Initiatives Foundation kwa nafasi yake katika kuwapa vijana jukwaa la kuonesha vipaji, ubunifu na uwezo wao.

Rais Samia amesema kupitia jukwaa hilo, vijana 15 wamepata heshima ya kipekee kutokana na ubunifu waliouonesha katika sanaa ya upigaji picha, ambapo kazi zao zilivutia hisia za wengi na baadaye kuuzwa kwa mamilioni ya fedha.

Aidha, Rais amesisitiza umuhimu wa kuendelea kuwaunga mkono vijana ili kupata ari, maarifa na ujuzi zaidi, hususan katika matumizi ya teknolojia, kwa lengo la kuongeza thamani ya kazi zao na kuwawezesha kunufaika kiuchumi kupitia vipaji na ubunifu wao.

Rais Samia pia amewashukuru na kuwapongeza wadau mbalimbali waliojitokeza kuunga mkono na kuchagiza shughuli hiyo, akizitaja taasisi za kifedha na wawekezaji katika sekta ya madini walioshiriki katika mnada wa picha zilizopigwa na vijana wa Kitanzania. Picha hizo zilibeba taswira ya maisha, utamaduni na fahari ya Zanzibar pamoja na Tanzania kwa ujumla.

Kwa upande wake, TIRA inaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kuwawezesha vijana kiuchumi na kuwahamasisha kutumia sanaa, ubunifu, ujuzi na teknolojia katika kujenga fursa za kujiajiri na kuongeza kipato.

Mamlaka inaamini kuwa uwezeshaji wa vijana na ulinzi wa ndoto zao kupitia vipaji na ujuzi ni sehemu muhimu ya kujenga kizazi chenye uwezo wa kujitegemea, kuchangia katika uchumi wa Taifa na kuongeza wigo wa mapato ya Serikali kupitia shughuli mbalimbali za uwekezaji zilizokingwa na Bima.

TIRA, Kwa Soko Salama la Bima