TIRA yazindua Ofisi ya Kanda Pemba; Kusogeza huduma za bima karibu na wananchi
ChakeChake, Pemba, Agosti 7, 2026
Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) leo imezindua rasmi Ofisi ya Kanda ya Pemba katika Jengo la Karafuu House, Chake Chake, ikiwa ni hatua muhimu ya kusogeza huduma za bima karibu zaidi na wananchi wa Visiwa vya Pemba na kuimarisha ukuaji wa sekta ya bima nchini.
Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Mheshimiwa Hemed Suleiman Abdulla, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mheshimiwa Hemed alisema kuwa kufunguliwa kwa Ofisi ya Kanda ya Pemba kutarahisisha upatikanaji wa huduma za bima kwa wananchi, wafanyabiashara na taasisi mbalimbali za Pemba, huku akiitaka TIRA kuendelea kutoa elimu ya bima ili kuongeza uelewa na ushiriki wa wananchi katika matumizi ya huduma za bima.
“Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki yanayowezesha sekta ya fedha, ikiwemo bima, kukua na kuchangia maendeleo ya uchumi pamoja na ustawi wa wananchi. Hivyo TIRA hakikisheni mnatoa elimu kwa wananchi mpaka wa vijijni ili kuwa na uelewa wa masuala ya bima” Alisema Mhe. Abdulla
Kwa upande wake, Kamishna wa Bima, Dkt. Baghayo Saqware, alisema uzinduzi wa Ofisi ya Kanda ya Pemba ni sehemu ya mkakati wa TIRA wa kusogeza huduma karibu na wananchi na kuongeza usimamizi wa sekta ya bima katika maeneo yote ya nchini.
Alieleza kuwa uwepo wa ofisi hiyo utasaidia kuongeza upatikanaji wa elimu ya bima, kuimarisha ulinzi wa watumiaji wa huduma za bima, kurahisisha usajili na usimamizi wa watoa huduma za bima pamoja na kushughulikia kwa wakati changamoto na malalamiko yanayohusu huduma za bima.
“TIRA itaendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kampuni za bima na wadau wengine kuhakikisha wananchi wa Pemba wanapata bidhaa na huduma za bima zinazokidhi mahitaji yao katika sekta mbalimbali ikiwemo kilimo, uvuvi, biashara, afya na mali” Alisisitiza Dkt. Saqware
Aidha, alisema kufunguliwa kwa ofisi hiyo kutasaidia kuongeza ushiriki wa wananchi katika huduma za bima na hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi wa Pemba na Zanzibar kwa ujumla.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, viongozi wa TIRA, wawakilishi wa kampuni za bima, taasisi za kifedha, viongozi wa dini, wafanyabiashara pamoja na wadau wengine wa sekta ya bima.
Uzinduzi wa Ofisi ya Kanda ya Pemba unaashiria dhamira ya TIRA ya kuendelea kuboresha upatikanaji wa huduma za bima nchini kwa kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, kwa wakati na karibu na maeneo wanayoishi na kufanya shughuli zao za kiuchumi.
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA
