Viongozi wa Vyama vya Ushirika Tabora Wahamasishwa Kuhusu Fursa Sekta ya Bima
Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) kupitia Kanda ya Magharibi, imetoa elimu ya bima tarehe 14 Septemba 2026 kwa viongozi wa vyama vya ushirika Manispaa ya Tabora, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa bima pamoja na kuhamasisha kuhusu fursa zilizopo katika sekta ya bima.
Katika elimu hiyo, viongozi hao wamehamasishwa kuhusu fursa mbalimbali zilizopo katika sekta ya bima, ikiwemo uwezekano wa vyama vya ushirika kusajiliwa na kutoa huduma za bima kwa wanachama wao. Hatua hiyo itasaidia kusogeza huduma za bima karibu na shughuli za kila siku za wanachama, hususan wakulima, pamoja na kupunguza changamoto ya uwepo wa bima feki katika sekta ya kilimo.
Meneja wa TIRA Kanda ya Magharibi, Bi. Awanje Matenda, ameeleza kuwa hatua inayofuata itakuwa ni kushuka moja kwa moja kwa wakulima kupitia vikao vya vyama vya ushirika vinavyotarajiwa kuanza hivi karibuni, ili kuwapatia elimu ya bima na kuwajengea uelewa kuhusu umuhimu wa kutumia huduma za bima zilizosajiliwa na zinazotambulika kisheria.
Aidha, elimu hiyo imekusudia kuwawezesha viongozi wa vyama vya ushirika kuwa mabalozi wa elimu ya bima kwa wanachama wao, hususan wakulima, na kuwasaidia kutambua fursa zilizopo katika sekta ya bima pamoja na kuchukua tahadhari dhidi ya bima feki.
TIRA Kwa Soko Salama la Bima
