TIRA yawanoa mawakala wa benki bima: Sheria, Miongozo na Kanuni zatajwa kuwa nyenzo muhimu.
Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imewataka Watumishi wa wakala wa benki bima wa NMB (Specified Persons) wanaoshughulika na biashara ya bima katika Kanda ya Kusini, kuendelea kuzingatia sheria, kanuni, miongozo na taratibu za uendeshaji wa biashara ya bima nchini kwenye Mafunzo yaliyofanyika tarehe 14 Oktoba 2026 katika ukumbi wa Tifan Hotel uliopo Mtwara Mjini.

Watumishi hao kutoka Matawi ya NMB Kanda ya Kusini ya Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma wamekumbushwa umuhimu wa kuwa na ujuzi na sifa stahiki za kitaalamu, pamoja na kuhakikisha uwepo wa Afisa Bima katika matawi yanayotoa huduma za bima.
Akizungumza katika mafunzo hayo, Bwn. Fabian Mbegete, Afisa Bima Mkuu, amewataka washiriki kuhakikisha wanatumia Rejista za Malalamiko na Madai kurekodi na kufuatilia malalamiko ya wateja kwa wakati, hata pale malalamiko yanapohusu kampuni au wakala mwingine wa bima.

Aliendelea kwa kuwakumbusha watumishi hao kuzingatia Ada za bima kwa kuhakikisha malipo ya bima yanatozwa kwa kuzingatia viwango vilivyowekwa katika Maelekezo ya Tozo ya Ada za chini za Bima, (Minimum Premium Rate Order (MRO) na matakwa mengine ya kisheria.
Mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za TIRA pamoja na NMB za kujenga uwezo wa Specified Persons na kuimarisha uendeshaji wa biashara ya bima kupitia mfumo wa Wakala wa benki bima, huku wakihakikisha wananchi wanapata huduma bora, sahihi, za uwazi na zinazozingatia sheria.
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA.
