TIRA yatoa elimu ya Bima ya Afya kwa Wote katika Jukwaa la Bima na Afya Dar es Salaam
Wananchi wameendelea kutembelea banda la Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) katika Jukwaa la Bima na Afya linalofanyika katika viwanja vya Posta Kijitonyama jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 20 hadi 24 Mei 2026. Katika jukwaa hilo, TIRA kama msimamizi wa utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake na umuhimu wa huduma za bima ya afya kupitia TIRA kanda ya Mashariki.
Akizungumza baada ya kutembelea banda la TIRA, Bi. Innosencia Abdallah, mkazi wa Wilaya ya Kinondoni, amesema amefurahishwa na elimu aliyopata kuhusu majukumu mbalimbali ya TIRA, ikiwemo kupokea na kushughulikia malalamiko yahusuyo bima pamoja na kufahamu fursa zilizopo katika sekta ya bima kama uwakala wa bima, udalali wa bima na huduma nyingine zinazohusiana na soko la bima.
Aidha, Meneja wa TIRA Kanda ya Mashariki, Bw. Kurenje Mbura, amesema jukwaa hilo limekuwa sehemu muhimu ya kuwafikia wananchi na kuwapatia elimu kuhusu usimamizi wa Bima ya Afya kwa Wote, ambapo takribani wananchi wamepatiwa elimu hiyo hadi sasa na pia wadau mbalimbali wameshiriki katika jukwaa hilo wakiwemo NHIF, kampuni ya bima ya Strategies na kampuni ya bima mtawanyo ya Pan Afrique Re.
Kilele cha tamasha hilo ni hapo kesho tarehe 24 Mei 2026, ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mhe. Albert Chalamila Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ambaye pia ataongoza ‘jogging’ maalum ya kuhamasisha masuala ya bima na afya. Jukwaa hilo limeandaliwa na FAGDI kwa kushirikiana na Wizara ya Afya.
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA
