Katibu Mkuu Wizara ya Afya apongeza ushirikiano wa TIRA na wadau wa sekta ya bima katika utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Grace Magembe, ametembelea Banda la Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) katika Kijiji cha Bima kinachoendelea kutoa huduma kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Saba Saba), na kupongeza ushirikiano uliopo kati ya TIRA na wadau wa sekta ya bima katika kuunga mkono utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote nchini.
Katika ziara hiyo, Katibu Mkuu alipata fursa ya kutembelea mabanda ya kampuni mbalimbali za bima ya afya zinazoshiriki katika Kijiji cha Bima, ambapo alielezwa kuhusu huduma wanazotoa pamoja na jitihada zinazofanywa kuwafikia wananchi kwa elimu na huduma za bima ya afya.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha usimamizi wa utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote ili kuhakikisha mfumo wa bima unaendelea kuwa wa haki, wenye uwazi na unaowajali wananchi wote pia amehimiza sekta ya bima kuendelea kuimarisha kitengo cha kupambana na udanganyifu katika bima (Insurance Anti-Fraud Unit), akieleza kuwa udhibiti wa vitendo vya udanganyifu utasaidia kulinda rasilimali za sekta hiyo, kuongeza uaminifu wa wananchi na kuhakikisha huduma za bima zinatolewa kwa ufanisi.
Kijiji cha Bima, kinachoratibiwa na TIRA, kinaendelea kuwa kitovu cha utoaji wa elimu na huduma za bima katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam, ambapo wananchi wanapata fursa ya kupata elimu, ushauri na huduma mbalimbali za bima kutoka kwa wadau wa sekta hiyo.
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA
