Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania

TIRA Logo
TIRA yasisitiza Mshikamano, Uwajibikaji na Ufanisi kwa Watumishi Wake
09 Feb, 2026
TIRA yasisitiza Mshikamano, Uwajibikaji na Ufanisi kwa Watumishi Wake

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imeendelea kusisitiza mshikamano, uwajibikaji na ufanisi katika utendaji kazi miongoni mwa watumishi wake, ikiwa ni msingi wa kufikia malengo ya taasisi na kuchangia maendeleo ya taifa.

Hayo yameelezwa leo Februari 9, 2026, wakati wa Kikao cha Kwanza cha Mkutano wa Nne wa Baraza la Nne la Watumishi wa TIRA kinachoendelea katika Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Nyerere, Kibaha mkoani Pwani. Kikao hicho kinalenga kujadili masuala mbalimbali yanayohusu maslahi ya watumishi, taasisi na taifa kwa ujumla.

Akifungua kikao hicho rasmi kwa niaba ya Mwenyekiti wa Baraza ambaye pia ni Kamishna wa Bima, Makamu Mwenyekiti wa Baraza na Naibu Kamishna wa Bima, Bi. Khadija I. Said, amewataka watumishi kuzingatia uwajibikaji na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao ili kufanikisha malengo ya Mpango Mkakati wa Mamlaka (CSP).

Bi. Khadija ameongeza kuwa utekelezaji bora wa majukumu utaiwezesha TIRA kuwa na rasilimali za kutosha kwa ajili ya kutekeleza bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ufanisi.

Kikao hicho kimehudhuriwa pia na wageni mbalimbali wakiwemo viongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa na Afya (TUGHE) Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na waalikwa kutoka ndani ya TIRA. Hadi sasa, mawasilisho mbalimbali yametolewa yakiwemo utekelezaji wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2025/2026, majukumu ya Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini (M&E) pamoja na wasilisho la Mkataba wa Huduma kwa Wateja.

Miongoni mwa ajenda kuu za kikao hicho ni kujadili vipaumbele vya bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 pamoja na kupitia na kujadili rasimu ya bajeti.Kikao hicho cha Baraza la Watumishi wa TIRA kinatarajiwa kuhitimishwa kesho Februari 10, 2026.

TIRA – Kwa Soko Salama la Bima