TIRA Kanda ya Unguja yakutana na wadau wa Skimu za Bima ya Afya Zanzibar
Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) Kanda ya Unguja, tarehe 20 Februari 2026 imekutana na wawakilishi wote wa Skimu za Bima ya Afya zinazohudumu Zanzibar kwa lengo la kujadiliana masuala mbalimbali hususani usajili wa Vituo vya Afya. Kikao hicho kimefayika kwenye ukumbi wa mikutano wa Ofisi za TIRA Unguja ambapo wawakilishi toka NHIF na kampuni za bima za Strategies, Jubilee, Britam na Assemble walihudhuria.
Mjadala huo umejikita zaidi kwenye usajili wa vituo vya Afya vilivyopo Zanzibar ambapo pamoja na changamoto mbalimbali ambazo zilitolewa na wajumbe wamekubaliana zoezi hilo kufanyika kwa vituo vyote ambavyo wanafanya navyo kazi. Aidha, TIRA imewakumbusha kuwa ni kosa kisheria kuendelea kufanya kazi na vituo ambavyo bado havijajisajili.
Pamoja na mjadala wa usajili wa vituo vya afya wadau wa Skimu za Bima Binafsi walieleza changamoto ya kutozwa gharama kubwa kwa huduma na vituo vya afya ukilinganisha na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF).
Kwenye utatuzi wa changamoto hiyo, walipendekeza Kamati ya kupanga Bei eekezi (Price list Committee) ikamilishe malengo yake iliyojiwekea mapema iwezekanavyo.
Kwenye kuhitimisha, wadau wamependekeza kuwe na kituo cha pamoja cha usajili (One stop center) ambapo TIRA, Wizara ya Afya na Mamlaka zingine zitakuwa zinasajili au kuhuisha leseni za vituo vya afya kwa pamoja.
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA
