Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania

TIRA Logo
TIRA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini yatoa elimu ya bima katika zoezi la ukaguzi wa vyombo vya moto
04 Mar, 2026
TIRA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini yatoa elimu ya bima katika zoezi la ukaguzi wa vyombo vya moto

TIRA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini yatoa elimu ya bima katika zoezi la ukaguzi wa vyombo vya moto

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi pamoja na wadau wa kampuni na mawakala wa bima imeshiriki zoezi la siku tatu la ukaguzi wa vyombo vya moto katika wilaya za Mbozi na Momba mkoani Songwe. Zoezi hilo limeanza tarehe 2 Machi 2026 katika eneo la Tunduma na limelenga kufanya tathmini ya utii wa Sheria ya bima za vyombo vya moto na kutoa elimu ya bima kwa watumiaji wa vyombo hivyo wakiwemo madereva na abiria.

Aidha, katika utekelezaji wa zoezi hilo, vyombo vya moto vilivyokutwa havina bima vimepatiwa fursa ya kukata bima papo hapo badala ya kupewa adhabu. Hata hivyo, wale waliokaidi agizo hilo wametozwa faini kwa mujibu wa sheria za usalama barabarani. Hatua hiyo imelenga kutoa nafasi kwa wananchi kutekeleza wajibu wao kwa hiari huku ikisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria.

Pia zaidi ya vyombo vya moto 800 vimekaguliwa vikihusisha bajaji, magari binafsi, malori ya mizigo na mabasi ya abiria. Idadi hiyo inaonesha mwitikio mkubwa wa wananchi na ushirikiano mzuri kati ya mamlaka, Jeshi la Polisi na wadau wa bima.

Meneja wa Kanda hiyo Bi. Neema Lutula ameeleza TIRA itaendelea kuimarisha utoaji wa elimu ya bima pamoja na kufanya kaguzi za mara kwa mara ili kuhakikisha sheria inazingatiwa na wananchi wanalindwa dhidi ya athari za ajali na majanga mbalimbali.
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA