Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania

TIRA Logo
Teknolojia yaongeza wigo wa huduma za bima nchini
27 Feb, 2026
Teknolojia yaongeza wigo wa huduma za bima nchini

Kamishna wa Bima, Dkt. Saqware, amesema kuwa TIRA imeendelea kuwafikia Watanzania na kuihudumia sekta ya bima kwa kutumia teknolojia za kisasa, hatua ambayo imeiwezesha kupunguza na kutatua changamoto za ufikiwaji na upatikanaji wa huduma za bima nchini. Amesema hayo katika Mkutano wa Mwaka 2026 wa Fintech Tanzania uilowakutanisha wadau wa teknolojia katika uchumi kwa lengo la kukuza ubunifu, ushirikiano na ujumuishwaji katika uchumi wa kidijitali wa Tanzania.

Amefafanua kuwa kupitia miongozo inayotolewa na TIRA, huduma za bima sasa zinapatikana kwa njia ya kidijitali kwa kutumia mifumo kama TIRAMIS na ORS, jambo linalochochea urahisi, upatikanaji mpana wa huduma, ubunifu pamoja na kuimarisha uzingatiaji wa kanuni ndani ya sekta ya bima. Hatua hiyo imeifanya sekta kuwa ya kisasa zaidi na inayokwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia.

Dkt. Saqware ameeleza kuwa ushiriki wa TIRA katika majukwaa kama ‘Fintech’ unasaidia kuibua fikra mpya na kubuni suluhu za kidijitali zenye tija kwa maendeleo endelevu ya sekta ya bima, huku pia ukichangia ukuaji wa uchumi kwa ujumla. Amesema majukwaa hayo yanatoa fursa ya kubadilishana uzoefu, kujifunza mwenendo wa teknolojia na kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za udhibiti, wabunifu na wadau wa uchumi wa kidijitali.

Vilevile, amebainisha kuwa ushiriki huo umeipa TIRA nafasi ya kutoa elimu na kujenga uelewa kuhusu masuala ya bima kwa wanafunzi, wabunifu wa teknolojia na wadau wa uchumi, hatua inayosaidia kukuza utamaduni wa matumizi ya bima miongoni mwa vijana na jamii kwa ujumla.

Akizungumza na vijana, Dkt. Saqware amewahimiza kujikita katika ubunifu wa mbinu na suluhu za kiteknolojia zenye kuleta tija kwa maendeleo ya taifa. Amesema bado kuna uhitaji mkubwa wa suluhu za kidijitali, hususan katika sekta za uchumi na bima. “Soko bado lipo na linahitaji suluhu hizo kuanzia katika miundombinu ya kidijitali, mifumo na hata ubunifu wa bidhaa za bima,” amesisitiza.

Aidha, ameongeza kuwa bado kuna pengo la muunganiko kati ya taasisi na vijana, jambo ambalo TIRA inalichukulia kwa uzito. Ameeleza kuwa taasisi inapanga kuanzisha majukwaa mbalimbali yatakayowawezesha vijana kushiriki, kutoa maoni, kuonesha ubunifu wao na kunufaika na fursa zilizopo ndani ya sekta ya bima, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na kukuza uchumi wa kidijitali nchini.