Mkutano wa Wanawake katika Sekta ya Fedha (TAWiFA): Naibu Kamishna wa Bima atoa wito kwa Wanawake kuwa Mabolozi wa Bima
Ili kujenga taifa bora na endelevu kiuchumi; Naibu Kamishna wa Bima kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), Bi. Khadija Said ametoa wito kwa Wanawake washiriki katika Mkutano wa Wanawake Sekta ya Fedha (TAWiFA) kuwa mstari wa mbele katika kuelimisha jamii kuhusu umuhimu na matumizi ya bidhaa mbalimbali za bima. Bi. Khadija amesema hayo leo Machi 23, 2026 katika mkutano unaoendelea hapa PAPU Tower, jijini Arusha.
Aidha, Naibu Kamishna amesema Mkutano huo unaoshirikisha wanawake kutoka sekta mbalimbali za kifedha kama benki, kampuni za bima, Taasisi za Serikali ni jukwaa muhimu kwa wanawake kubadilishana uzoefu, kujenga mambo ya kitaaluma na kuweka mikakati ya pamoja katika nafasi ya mwanamke kiuchumi.
Mbali na hayo, Bi. Khadija amewataka wanawake kuongeza maarifa na ujuzi hasa eneo la kifedha kwa kujifunza zaidi huku wakitumia ubunifu na teknolojia katika kukuza sekta mbalimbali ikiwemo ya bima ili elimu iweze kuwafikia wanawake wengi wa mjini na vijijini na pia wenye vipato tofauti tofauti.
Wanawake kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) na Ofisi ya Msuluhishi wa Migogoro ya Bima (TIO) wanashiriki Wiki ya Wanawake katika Sekta ya Fedha ambayo imeanza Machi 22, 2026 kwa utoaji elimu ya fedha kwa wanawake wajasiriamali Arusha na hapo kesho kutakuwa na zoezi la upandaji kuunga mkono juhudi za Serikali katika kupambana na mabadiliko ya tabianchi.
#MachinaWanawakeSektayaFedha
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA
