Mafunzo ya Bima kwa Waandishi wa Habari yafanyika Zanzibar
Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) kupitia Kanda ya Unguja na Ofisi ya Zanzibar na kwa kushirikiana na Ofisi ya Msuluhishi wa Migogoro ya Bima Tanzania (TIO) jana tarehe 3 Machi 2026 imefanya mafunzo kuhusu bima kwa Waandishi wa Habari kwa lengo la kuowaongezea uweledi wa kuripoti taarifa mbalimbali kuhusu bima.
Mafunzo hayo yaliyofanyika katika Ukumbi ZSSF yalihudhuriwa na Waandishi tisini na sita (96) kutoka vyombo vya habari arobaini (40) vilivyopo Unguja.
Akifungua mafunzo hayo Naibu Kamishna wa Bima Tanzania Bi. Khadija Saidi aliwaeleza washiriki namna TIRA inavyoendesha shughuli zake na hatua ambayo imepiga katika kuendeleza soko la bima nchini. Aidha, aliwataka washiriki kuwa mabalozi wazuri kwa elimu ambayo watakayoipata ili kuendelea kuongeza wigo wa watumiaji wa bima nchini ikiwemo wao wenyewe.
Kwa upande wake Meneja wa Kanda ya Unguja Bw. Kurenje Mbura alizungumzia shughuli zinafanywa na ofisi hiyo pamoja kueleza fursa zinazopatikana kwenye Bima. Pia aliwaomba Waandishi kuwasisitiza wananchi kukata Bima kwa watoa huduma wenye leseni hai zilizotolewa na TIRA.
Naye Msajili wa Migogoro toka ofisi ya TIO Wakili Jamal Mwasha alitoa mada kuhusu uwepo wa ofisi hiyo na namna ambavyo inashughulikia migogoro na kueleza tofauti ya kiutendaji baina ya TIO na TIRA.
Mada nyingine zilizotolewa ni kuhusu Bima na bidhaa zake, mifumo ya TEHAMA inayotumiwa na TIRA, fursa ambazo zinapatikana kwenye Bima, faida za Bima na changamoto mbalimbali zinazolikabili soko la Bima nchini.
Washiriki walipatiwa nafasi ya kuchangia ambapo pamoja na kuuliza maswali mbalimbali pia walitoa ombi la kupewa mafunzo hayo mara kwa mara ili kuendelea kuwaongezea uelewa. TIRA imeahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano.
