Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania

TIRA Logo
Filamu ya Koti Jeupe yazinduliwa: Sanaa yatumika kukuza elimu ya Bima ya Maisha
18 Feb, 2026
Filamu ya Koti Jeupe yazinduliwa: Sanaa yatumika kukuza elimu ya Bima ya Maisha

Filamu ya Koti Jeupe yazinduliwa: Sanaa yatumika kukuza elimu ya Bima ya Maisha

Simulizi ya kusisimua, visa na mikasa vilivyopangwa kwa ustadi—hadithi iliyosimuliwa kwa umahiri kuhusu uhalisia wa maisha ya kila siku katika matumizi ya bima—ndiyo kiini cha filamu ya Koti Jeupe iliyozinduliwa tarehe 17 Februari 2026 katika Ukumbi wa Dar Century Cinemax jijini Dar es Salaam. Filamu hiyo inaangazia saga ya familia na kuonesha kwa undani umuhimu wa bima ya maisha kama ulinzi kwa familia na jamaa. 

Kupitia ubunifu wa kampuni za bima nchini, wazo hili limewekwa katika picha na sauti za kuvutia likiwa na lengo la kuelimisha Watanzania kuhusu umuhimu wa bima ya maisha kwa kutumia sanaa ya uigizaji. Ndani ya filamu hiyo, mtazamaji anakutana na visa alivyopitia binti mdogo Amanda, na namna bima ya maisha kutoka kwa mzazi wake ilivyokuwa nguzo ya matumaini na usalama baada ya changamoto zisizotarajiwa

Aidha, Mgeni rasmi katika uzinduzi huo; Kamishna wa Bima Dkt. Baghayo A.  Saqware amepongeza waandaaji na waigizaji kwa utekelezaji wa kazi kubwa katika kuelimisha umma kwa njia hiyo rahisi. Uzinduzi huo pia ulihudhuriwa na viongozi kutoka ATI, kampuni za bima na wadau wengine mbalimbali.

Utoaji elimu kwa umma kupitia njia mbalimbali kama filamu, semina, warsha na vyombo vya habari ni sehemu ya kipaumbele cha TIRA ili wananchi wengi wafahamu umuhimu wa bima na kuzitumia bidhaa mbalimbali za bima katika kujikinga na majanga yasiyotarajiwa na hatimaye kulinda familia zao kwa bima ya maisha, afya , mali na uwekezaji.