The United Republic of Tanzania

Tanzania Insurance Regulatory Authority

“TIRA kwa Soko Salama la Bima”
Elimu ya Bima Yawapa Mwanga Wananchi Maonesho ya Nane Nane Dodoma
04 Aug, 2026
Elimu ya Bima Yawapa Mwanga Wananchi Maonesho ya Nane Nane Dodoma

 

Agosti 4, 2026

Wananchi wanaotembelea banda la Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) katika Maonesho ya Wakulima Nane Nane yanayoendelea Viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma, wanaendelea kupata elimu kuhusu huduma na bidhaa mbalimbali za bima, hatua inayowasaidia kuelewa namna bima inavyoweza kulinda maisha, biashara na shughuli za uzalishaji dhidi ya vihatarishi mbalimbali.

Miongoni mwa wanufaika wa elimu hiyo ni Bw. Sylvester Msindo, mhandisi ambaye alisema elimu aliyoipata kuhusu bima ya uhandisi imempa uelewa mpya wakati huu akiwa katika maandalizi ya kufungua kampuni yake. Alieleza kuwa sasa anatambua umuhimu wa bima katika kulinda miradi, vifaa na shughuli za ujenzi, jambo litakalomsaidia kuanzisha biashara yake kwa msingi imara wa usimamizi wa hatari

"Nimepata mwanga mkubwa kuhusu bima ya uhandisi. Sikujua kwamba inaweza kuwa sehemu muhimu ya kulinda uwekezaji wangu tangu hatua za mwanzo za kuanzisha kampuni," alisema Bw. Msindo, huku akiwahimiza wataalamu na wajasiriamali wengine kutafuta elimu ya bima kabla ya kuanzisha miradi yao.

Aidha, wakulima wanaotembelea banda la TIRA wameendelea kupata elimu kuhusu bima ya kilimo, ikiwemo namna inavyoweza kuwakinga dhidi ya hasara zinazotokana na ukame, mafuriko, magonjwa ya mazao na mifugo pamoja na vihatarishi vingine vinavyoathiri uzalishaji. Wengi wao walieleza kuwa hawakufahamu kuwa huduma za bima zinapatikana pia kwa sekta ya kilimo hadi walipotembelea banda hilo.

Kupitia ushiriki wake katika Maonesho ya Nane Nane, TIRA inaendelea kuwafikia wananchi wa kada mbalimbali kwa elimu ya bima inayolenga kuongeza uelewa, kuhamasisha matumizi ya bima na kujenga jamii yenye uwezo wa kukabiliana na vihatarishi kupitia huduma za bima.

TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA