Elimu ya Bima Yaendelea Kuwafikia Wananchi Kupitia Redio Mashujaa Lindi.
Elimu ya Bima Yaendelea Kuwafikia Wananchi Kupitia Redio Mashujaa Lindi.
Watumishi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania kutoka Ofisi ya Kanda ya Kusini iliyopo Mkoani Lindi, inayohudumia Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma, wametoa elimu ya bima tarehe 21/Mei/2026, kupitia Redio Mashujaa kwa lengo la kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu huduma za bima na majukumu ya Mamlaka kwa ujumla.
Akizungumza kwenye kipindi hicho, Bi. Tabia Mchakama, Afisa Uhusiano kwa Umma Mkuu, alieleza majukumu ya Mamlaka pamoja na mtawanyo wa ofisi za TIRA nchi nzima ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma kwa ukaribu zaidi.
Naye Bwana Fabian Mbegete, Afisa Bima Mkuu alitoa elimu kuhusu sheria za bima za lazima ikiwemo bima ya vyombo vya moto, bima ya petroli, bima ya Vivuko na bima ya majengo yenye mikusanyiko ya watu wengi.
Katika kipindi hicho, TIRA iliungana na Afisa Mwandamizi Ndugu Tumaini Geofrey Nyingi kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) ambaye alieleza utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote na umuhimu wake kwa wananchi.
Kupitia kipindi hicho cha Redio simu nyingi za papo kwa hapo zilipigwa kutoka kwa wananchi wakiuliza maswali mbalimbali kwa ajili ya kupata ufafanuzi zaidi ambapo maafisa walijibu kwa ufasaha.
Elimu hiyo ni sehemu ya juhudi za kuendelea kuwafikia wananchi na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa bima nchini.
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA.
