Elimu ya bima ya kilimo na bima ya afya yatolewa kwa wakulima wa kijiji cha Mtiniko, mkoani Mtwara.
Wakulima wanaohudumu kupitia vyama vya msingi vya ushirika (AMCOS) wamepokea mafunzo muhimu juu ya bima ya kilimo na bima ya afya, yaliyotolewa mnamo tarehe 19 Februari 2026, na Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) kupitia Ofisi yake ya Kanda ya Kusini inayohudumia Mikoa ya Lindi, Ruvuma na Mtwara.
Katika mkutano uliofanyika kijijini hapo, Meneja wa TIRA Kanda ya Kusini, Bwn. Salum Yungwa aliwaeleza wakulima hao umuhimu wa kukatia bima ya kilimo kwa mazao na mifugo, ikiwemo namna bima inavyoweza kuwasaidia kukabiliana na hatari za asili kama mvua nyingi kupita kiasi zisizotarajiwa, ukame, magonjwa ya mimea na wadudu waharibifu.
Aidha, wakazi hao pia walipatiwa elimu ya Bima ya Afya kwa Wote, ikiwa ni mpango wa kitaifa wa Serikali chini ya Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan unaolenga kuhakikisha wananchi wanapatiwa huduma bora za afya bila kikwazo cha gharama kubwa.
Watendaji wa Mamlaka walioongoza mjadala huo kwa kusisitiza kwamba bima sio tu nyenzo ya kukabiliana na hasara bali ni sehemu ya kujenga utulivu wa kifedha kwa wakulima na familia zao endapo kutatokea majanga yasiyotabirika akiwa shambani au nyumbani. Ushirikiano uliendelea hadi kwa maelezo ya jinsi ya kujiandikisha kwenye huduma na taratibu za kukata bima kupitia vyama vya ushirika (AMCOS) ili kupata manufaa bora kwa pamoja.
Baadhi ya wakulima walitoa shukrani kwa juhudi hizo, wakisema elimu hiyo itawasaidia kupanua fursa za kupata fidia pindi msimu wa uzalishaji ukikikumbwa na changamoto hasa kwa upande wa zao la korosho ambalo ndilo linalolimwa kwa kiasi kikubwa katika maeneo yao na kwamba sasa wataanza kuchukua hatua za kukata bima kabla ya kufikiwa na hasara.
Mamlaka imeongeza juhudi za uhamasishaji bima nchini kote, ikilenga kujenga utamaduni wa kutumia bidhaa za bima kama chombo cha kulinda uwekezaji na ustawi wa kaya za wakulima na wananchi kwa ujumla.
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA
