Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania

TIRA Logo
Dkt. Saqware: Tuzo za ATI Zimekuja Wakati Muhimu kwa Ukuaji wa Sekta ya Bima.
24 May, 2026
Dkt. Saqware: Tuzo za ATI Zimekuja Wakati Muhimu kwa Ukuaji wa Sekta ya Bima.

Kamishna wa Bima nchini Tanzania Dkt. Baghayo Saqware amesifu ubunifu uliotumika katika kuanzishwa kwa Tuzo za Bima za ATI zilizofanyika tarehe 22 Mei, 2026 katika ukumbi wa The Super Dome kwani zimekuja katika wakati muhimu kwa taifa na Tasnia ya Bima nchini.

Aidha, amesema tukio hilo ni kubwa na la kihistoria kufanyika nchini Tanzania na kwamba ni hatua muhimu ya ukuaji wa Sekta ya Bima na mchango wake kwa Pato la Taifa.

Pia Dkt. Saqware akihutubia mamia ya washiriki katika usiku wa Tuzo za Bima za ATI kwa mwaka 2026 amesema katika ulimwengu wa kisasa wa uchumi hakuna anayeweza kuwekeza bila uwepo wa Bima ambayo hukinga ustawi na usalama wa mali zao.

Tuzo hizo zilizoandaliwa na ATI (Association of Tanzania Insurers) ziliwakutanisha wadau wa sekta ya fedha, kampuni za bima, brokers pamoja na washirika mbalimbali wa tasnia ya bima kwa lengo la kutambua mchango wa wabunifu, viongozi na taasisi zinazofanya vizuri katika sekta hiyo. Hafla hiyo pia ilitafsiriwa kama hatua mpya ya kuhamasisha ushindani wenye tija na utoaji bora wa huduma za bima nchini.

Katika hafla hiyo, washiriki walisisitiza umuhimu wa kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu huduma za bima pamoja na matumizi ya teknolojia katika kuboresha huduma kwa wateja huku akisusitiza uadilifu. Aidha, viongozi mbalimbali waliohudhuria walieleza kuwa ukuaji wa sekta ya bima utaendelea kuwa nguzo muhimu katika kuimarisha uchumi wa taifa na kuwapa wananchi uhakika wa kifedha wanapokumbwa na majanga au changamoto zisizotarajiwa.

Tukio hilo limevuta hisia za wadau wengi wa sekta ya bima nchini kutokana na umuhimu wake katika kukuza tasnia hiyo na kuhamasisha ubora wa huduma katika soko la bima Tanzania.

TIRA, Kwa Soko Salama la Bima