Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania

TIRA Logo
Uelimishaji wa bima kwa njia ya fasihi: Visa na Mikasa kumi na moja vyaandikwa 
28 May, 2025
Uelimishaji wa bima kwa njia ya fasihi: Visa na Mikasa kumi na moja vyaandikwa 

Leo Mei 28, 2025 Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania imeshuhudia uzinduzi wa vitabu kumi na moja (11) vyenye hadithi za kusisimua kuhusu umuhimu, mafanikio na mafunzo ya bima kwa jamii. Tukio hilo lililoandaliwa na Tanzania Fasihi Fund (TAFF) limefanyika katika viwanja  vya Kijiji cha Makumbusho Dar es Salaam.

Vitabu hivyo vimeandikwa na waandishi mahiri kutoka Tanzania na nchi jirani. Baadhi ya majina ya vitabu hivyo ni pamoja na Hazina, Fanikio Aridhini, Kibaruani, Kiburi si Muungwana, Najutia nafasi, Joto na Jasho baharini, Bima Mujarabu, Hazina ya Ukaidi na vingine mbalimbali. 

Akitoa neno la Shukrani katika Tamasha hilo la tatu la Fasihi Mkurugenzi wa TAFF, Bw. Hussein Wamaiya ameishukuru TIRA kwa kuonyesha njia katika kuunga mkono kazi za sanaa na kuzitumia kama njia ya kuelimisha jamii kuhusu bima. Lakini pia kuwa mdhamini mkubwa katika tamasha hilo. 

Aidha, kwa upande wa Mamlaka ikiwakilishwa na Meneja wa Uhusiano na Mawasiliano, Bi. Hadija Maulid kwa niaba ya Kamishna wa Bima ameushukuru uongozi wa TAFF kwa heshima waliyoipa TIRA na sekta ya bima kwa ujumla na kusisitiza lengo la sekta ya bima ni kufikia azma ya Serikali kuwa ifikapo mwaka 2030  kupata asilimia 80 ya watanzania wenye uelewa kuhusu bima na asilimia 50 ya wanaotumia bima hivyo njia mbalimbali za kuelimisha zinatumika kufikia lengo hilo.

Vitabu hivyo vitachapishwa na kusambazwa sehemu mbalimbali kama maktaba, mashuleni na vyuoni ili kukuza uelewa wa bima kwa jamii.

TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA