The United Republic of Tanzania

Tanzania Insurance Regulatory Authority

“TIRA kwa Soko Salama la Bima”
TIRA Kanda ya Kaskazini yajadili fursa za ukuaji wa Soko la Bima
20 Sep, 2026
TIRA Kanda ya Kaskazini yajadili fursa za ukuaji wa Soko la Bima

Ofisi ya Kanda ya Kaskazini ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), tarehe 18 Septemba 2026, imefanya kikao kazi na wadau wa sekta ya bima, wakiwemo Mameneja wa Matawi (Branch Managers) kutoka kampuni mbalimbali za bima zinazofanya kazi katika Kanda hiyo. Kikao hicho kililenga kujadili fursa mbalimbali za maendeleo zilizopo katika Kanda ya Kaskazini na namna zinavyoweza kutumika kukuza matumizi ya bidhaa za bima miongoni mwa wananchi.

Akizungumza katika kikao hicho, Meneja wa Kanda ya Kaskazini, Dkt. Emmanuel Lupilya, amezitaka kampuni za bima kuhakikisha zinashughulikia na kulipa madai halali ya wateja kwa wakati ili kuimarisha imani ya wananchi katika huduma za bima na kuongeza matumizi ya bidhaa za bima.

Aidha, amewahimiza wadau kuwa wabunifu katika kubuni na kuboresha bidhaa za bima zinazokidhi mahitaji ya soko la sasa, kwa kuzingatia ukuaji wa shughuli za kiuchumi katika Kanda hiyo na fursa zinazojitokeza katika sekta mbalimbali.

Vilevile, Dkt. Lupilya amesisitiza umuhimu wa wadau kutumia fursa zitakazotokana na kufanyika kwa Mkutano wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) utakaofanyika jijini Arusha mwezi Oktoba 2026, kwa kuandaa huduma na bidhaa za bima zinazoweza kukidhi mahitaji yatakayojitokeza kutokana na shughuli za mkutano huo.