TIRA yatoa Elimu ya Bima na kuibua fursa za Biashara kwa Utumishi SACCOS - Unguja
TIRA yatoa Elimu ya Bima na kuibua fursa za Biashara kwa Utumishi SACCOS - Unguja
Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) Kanda ya Unguja tarehe 25 Agosti 2026 imefanya kikao maalum na Uongozi wa Utumishi SACCOS kwa lengo la kutoa elimu ya kina kuhusu masuala ya bima pamoja na kuainisha fursa za biashara na uwekezaji zinazopatikana katika sekta ya bima.
Kikao hicho kimelenga kuwajengea uelewa viongozi wa SACCOS kuhusu aina mbalimbali za bima, majukumu ya TIRA na namna chama hicho kinavyoweza kutumia fursa zilizopo katika sekta ya bima kama sehemu ya kuongeza vyanzo vya mapato na kukuza shughuli zake za uwekezaji.
Meneja wa TIRA Kanda ya Unguja Bw. Said Salum aliueleza Uongozi wa SACCOS majukumu ya Mamlaka huku akisisitiza umuhimu wa uelewa wa bima katika kuchangamkia fursa zinazotokana na ukuaji wa sekta hiyo.
Naye, Afisa Bima wa TIRA Kanda ya Unguja, Bw. Adam Magori, ametoa elimu kuhusu aina mbalimbali za bima na kueleza kwa kina fursa ya biashara ya uwakala wa bima, ikiwemo namna ya kuanzisha uwakala, uendeshaji wake na mfumo wa mgawanyo wa kamisheni katika aina mbalimbali za bima.
Kupitia elimu hiyo, Uongozi wa Utumishi SACCOS ulionesha nia ya kuchunguza uwezekano wa kuanzisha uwakala wa bima kama moja ya shughuli za uwekezaji na vyanzo vya mapato vya SACCOS.
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA
