TIRA yatoa elimu ya bima katika maonesho ya wakulima viwanja vya Ipuli Tabora
TIRA yatoa elimu ya bima katika maonesho ya wakulima viwanja vya Ipuli Tabora
Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) kupitia Kanda ya Magharibi inaendelea kutoa elimu ya bima kwa wananchi wanaotembelea Maonesho ya Wakulima yanayoendelea katika Viwanja vya Ipuli, mkoani Tabora, leo tarehe 6 Agosti 2026. Elimu hiyo inalenga kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa bima katika kulinda maisha, mali na shughuli mbalimbali za kiuchumi, hususan sekta ya kilimo.
Akizungumza katika maonesho hayo, Meneja wa Kanda ya Magharibi, Bi. Awanje Matenda, amewahimiza wananchi, hususan wakulima na wafugaji, kutembelea banda la TIRA ili kujipatia elimu sahihi kuhusu huduma za bima na manufaa yake katika kulinda uwekezaji wao.
"Kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wetu, hivyo ni muhimu wakulima wakafahamu fursa zinazotolewa na bima ya kilimo. Bima huwasaidia kupunguza athari za hasara zinazoweza kusababishwa na majanga mbalimbali na kuwawezesha kuendelea na uzalishaji kwa kujiamini," amesema Bi. Matenda.
TIRA inaendelea kuwakaribisha wananchi wote kutembelea banda lake katika Viwanja vya Ipuli ili kupata elimu ya bima bila malipo, kuuliza maswali na kupata ufafanuzi kuhusu huduma mbalimbali za bima zinazopatikana nchini, kwa lengo la kujenga jamii yenye uelewa mpana wa masuala ya bima na kuongeza matumizi ya huduma hizo kwa maendeleo ya uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.
TIRA kwa Soko Salama Bima
