The United Republic of Tanzania

Tanzania Insurance Regulatory Authority

“TIRA kwa Soko Salama la Bima”
TIRA yatoa elimu ya Bima Jukwaa la LCCF 2026
26 Jul, 2026
TIRA yatoa elimu ya Bima Jukwaa la LCCF 2026

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania @tira_tz imeshiriki katika Jukwaa la Tano la Utekelezaji wa Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (LCCF 2026) kwa kutoa elimu kuhusu umuhimu wa bima katika kuimarisha ustahimilivu na uendelevu wa shughuli za madini nchini.

Akizungumza katika jukwaa hilo, Meneja wa TIRA Kanda ya Ziwa, Bw. Oyuke Phostine @oyukephostine amesema bima ni nyenzo muhimu inayosaidia sekta ya madini kuendelea kufanya kazi hata inapokumbwa na majanga au hatari zisizotarajiwa kwa kupunguza athari za kifedha.

Amesema kuna zaidi ya aina 18 za vihatarishi vinavyoweza kukingwa kupitia bima, ikiwemo urejeshwaji wa mazingira baada ya uchimbaji, ajali kazini, moto, uharibifu wa mitambo na madai ya dhima kwa watu wengine.

Bw. Oyuke amesisitiza kuwa matumizi sahihi ya huduma za bima yanasaidia usimamizi wa vihatarishi na kuimarisha sekta ya madini, huku TIRA ikiendelea kuhakikisha watoa huduma za bima wanabuni kinga zinazokidhi mahitaji ya sekta hiyo.

Jukwaa la LCCF 2026 limewakutanisha wadau wa sekta ya madini, taasisi za umma na binafsi pamoja na watoa huduma mbalimbali kujadili namna ya kuongeza ushiriki wa Watanzania katika shughuli za madini, huku TIRA ikiendelea kuhamasisha matumizi ya bima kulinda uwekezaji na kukuza maendeleo endelevu.