TIRA yapongeza IAAT kwa mchango wake ukuaji soko la bima na ongezeko la ajira nchini
Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imetoa pongezi hizo katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakala wa Bima Tanzania (IAAT) ambao umefanyika leo Agosti 20, 2026 katika Ukumbi wa EALCC, Ubungo, Dar es Salaam; akitoa neno Meneja wa TIRA Kanda ya Mashariki, Bw. Kurenje Mbura, kwa niaba ya Kamishna wa Bima,pia amesema mawakala wana nafasi muhimu katika kuifikisha bima kwa wananchi na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa huduma hiyo.
Aidha, amesema sekta ya bima inapoendelea kukua, shughuli za uwakala zinaendelea kutoa fursa kwa Watanzania, hususan vijana, kujiajiri na kupata ajira katika sekta ya bima lakini zaidi uwepo wa mawakala katika maeneo mbalimbali nchini unasaidia kuunganisha wananchi na kampuni za bima, hivyo kuongeza upatikanaji wa huduma na kuchangia upanuzi wa soko.
Kwa upande wake, Bw. Lugano Mkisi ambaye ni Mwenyekiti wa Chama hicho wakati wa hotuba yake mbele ya Mgeni Rasmi Kaimu Naibu Katibu Mkuu na Kamishna wa Idara ya Fedha za Nje, Wizara ya Fedha Bw. Rished Badu akimuwakilisha Waziri wa Fedha,ameeleza mafanikio, changamoto na fursa za Chama hicho. Ambapo hadi sasa chama kimefanikiwa kukuza idadi ya wanachama kutoka 200 hadi 1,178 wakati chama kinaanzishwa,kuwajengea uwezo wanachama kwa mafunzo na kuboresha katiba ya chama.
Aidha Bw. Mkisi amesema chama hicho kimeendeleza ushirikiano thabiti na TIRA kama mlezi wao, pamoja na kuanzisha Uhusiano na ushirikiano kwa kuingia makubaliano (MOU) na LATRA pamoja na NHIF katika kuunga mkono jitihada za Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika utekelezaji wa bima ya afya kwa Wote (UHI).
Katika maombi yao kwa Serikali IAAT wamewasilisha masuala mbalimbali ambayo Bw. Badu amekiri kupokea na kwa kushirikiana na TIRA changamoto mbalimbali zinazowakabili kutatuliwa.
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA
