TIRA yapokea maoni ya wadau masuala ya Udhibiti Udanganyifu katika Bima
Leo tarehe 2 Septemba 2026, TIRA kupitia Kitengo cha Udhibiti Udanganyifu imefanya kikao kazi na kampuni za bima lengo likiwa ni kupokea maoni na kujadili masuala mbalimbali ya Rasimu ya Mwongozo wa Udhibiti Udanganyifu ambao utatumika katika kutekeleza mapambano ya masuala hayo katika sekta ya bima.

Mwenyekiti wa kikao hicho; Kamishna wa Bima Tanzania Dkt. Baghayo Saqware ametoa wito kwa kampuni za bima kushirikiana na TIRA katika kudhibiti udanganyifu katika soko lakini na kuendelea kujielimisha kuhusu masuala ya udanganyifu katika bima. Kamishna pia amesisitiza juu ya uaminifu wa watumishi hao ili kulinda sekta ya bima kwa kujiepusha na vitendo vya udanganyifu katika soko.

Aidha, Ofisi ya Mashtaka Mkoa wa Dar es Salaam (NPS) imeshiriki kwa kutoa elimu kwa watoa huduma hao kuhusu makosa ya jinai yanayotokana na shughuli za biashara ya bima nchini yakiwemo kuhusu udanganyifu katika bima pia wametoa rai kutoa taarifa za udanganyifu katika soko ili wahusika washughulikiwe na vyombo vya sheria.

Naye, Meneja Udhibiti Udanganyifu TIRA Bw. Okoka Jailo Mgavilenzi amesema kikao hicho kimekuwa cha mafanikio makubwa kwa kupokea maoni na mapendekezo mengi ambayo yataboresha mwongozo huo na sekta itapata mwongozo ambao ni jumuishi kwa kuzingatia maoni ya sekta na siku za hivi karibuni mwongozo huo utatolewa kwa ajili ya matumizi ya soko, wadau wote wa biashara ya bima pamoja na wananchi kwa jumla. Zaidi Mwongozo huo utaeleza kuhusu kugundua, kuzuia na kutoa taarifa za udanganyifu.
#Toa taarifa za udanganyifu katika bima
#Udanganyifu katika bima ni kosa la jinai
TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA
