TIRA yamuaga Mkt. wa Mabalozi wa Bima Mhandisi Zena Said, yapongeza mchango wake katika kukuza Sekta ya Bima
Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) leo Agosti 21, 2026 imefanya hafla fupi ya kumuaga Mhe. Balozi Mhandisi Zena A. Said, ambaye amekuwa Mwenyekiti wa Mabalozi wa Bima tangu mwaka 2023, huku ikimpongeza kwa mchango wake katika kuhamasisha matumizi ya bima na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu sekta ya bima.
Akizungumza katika hafla hiyo, Balozi Zena A. Said – Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Saudi Arabia; amesema kupitia nafasi aliyoitumikia kama Balozi wa Bima amejifunza mengi, ikiwemo mafunzo kuhusu bima na utatuzi wa migogoro. Ameipongeza TIRA kwa kazi nzuri inayofanya kwa kushirikiana na kampuni za bima, huku akihimiza kuendelea kutengeneza bidhaa na vifurushi vinavyokidhi mahitaji ya Watanzania, akitolea mfano Takaful inayozingatia misingi ya Sharia
Aidha, Kamishna wa Bima Dkt. Saqware ametaja mafanikio mbalimbali yalipotikana chini ya uongozi wa Balozi Zena ikiwemo kusukuma ajenda ya bima ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Baraza la Wawakilishi na kuwaomba mabalozi wote kuendelea kuwa chachu ya maendeleo ya sekta ya bima nchini.
Kwa upande wake, Msuluhishi wa Migogoro ya Bima, Bi. Margaret Mngumi, amemshukuru kiongozi huyo kwa hekima, uvumilivu na mchango wake katika kuimarisha ushirikiano na maridhiano ndani ya sekta ya bima. Pia Bi. Flora Minja akizungumza kwa niaba ya ATI amemshukuru Mhe. Zena kwa uongozi wake thabiti na kuahidi ushirikiano na Mkt. wa Mabalozi mpya katika masuala ya bima.
Nae Naibu Kamishna wa Bima Bi. Khadija Said, amemshukuru Balozi Zena kwa kwa kujitoa kwake katika shughuli mbalimbali za TIRA, na kuahidi kuendeleza kazi njema aliyoianza kwa kiongozi mpya na Mwenyekiti wa Mabalozi wa Bima ambaye ni Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), Mansura Mossi Kassim.
