The United Republic of Tanzania

Tanzania Insurance Regulatory Authority

“TIRA kwa Soko Salama la Bima”
TIRA yaimarisha uwezo wa maafisa wa Kanda katika kudhibiti udanganyifu
04 Sep, 2026
TIRA yaimarisha uwezo wa maafisa wa Kanda katika kudhibiti udanganyifu

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imeendelea kuimarisha uwezo wa Maafisa wake wa Kanda katika kutambua, kuzuia na kuripoti matukio ya udanganyifu wa bima, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa jitihada za kuimarisha udhibiti wa vihatarishi vya udanganyifu katika soko la bima.


Akitoa mafunzo kuhusu udhibiti wa udanganyifu wa bima, Meneja wa Udhibiti wa Udanganyifu wa Bima wa TIRA, Bw. Okoka Jairo Mgavilenzi, alisema elimu na uhamasishaji kwa watumishi wa TIRA ni muhimu katika kuhakikisha wanakuwa mstari wa mbele katika utekelezaji wa juhudi za kupambana na udanganyifu wa bima.

Bw. Mgavilenzi alieleza kuwa Maafisa wa Kanda wana nafasi muhimu katika kutekeleza udhibiti huo, hususan katika kufanya uhakiki wa kina (due diligence) wakati wa usajili wa mawakala wa bima, ili kuepusha kusajili watu wasio na sifa zinazostahili au wenye vihatarishi vinavyoweza kuathiri uadilifu wa soko la bima.

Miongoni mwa maeneo yaliyopewa kipaumbele katika mafunzo hayo ni udanganyifu unaoweza kujitokeza katika bima za vyombo vya moto, bima za mali na moto, bima ya afya na bima za maisha yakiainishwa kama maeneo ambayo yanahitaji umakini wa karibu kutokana na vihatarishi vya udanganyifu vinavyoweza kujitokeza katika utekelezaji wa utoaji huduma za bima.

Kwa upande wake, Afisa Tehama wa TIRA, Bw. Paul Nicholaus, alisema maendeleo ya teknolojia yameleta changamoto mpya katika udhibiti wa udanganyifu, ambapo baadhi ya watu hutumia teknolojia katika kughushi taarifa na nyaraka mbalimbali zinazohusiana na huduma za bima.

Kupitia mafunzo haya, uwezo wa Maafisa wa Kanda wataweza kutambua viashiria vya udanganyifu, kuzuia matukio yanayoweza kujitokeza na kuripoti masuala ya udanganyifu kwa wakati ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa. Hatua hii inatarajiwa kuimarisha uwezo wa TIRA katika ngazi ya Kanda sambamba na kuendelea kulinda uadilifu na usalama wa soko la bima nchini.