The United Republic of Tanzania

Tanzania Insurance Regulatory Authority

“TIRA kwa Soko Salama la Bima”
TIRA yafanya Mabadilishano ya Uzoefu na Taasisi za Bima kutoka Zimbabwe
26 Aug, 2026
TIRA yafanya Mabadilishano ya Uzoefu na Taasisi za Bima kutoka Zimbabwe

TIRA Yafanya Mabadilishano ya Uzoefu na Taasisi za Bima kutoka Zimbabwe

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imepokea ujumbe wa wageni kutoka Zimbabwe kwa ajili ya kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu masuala mbalimbali ya usimamizi na uendelezaji wa sekta ya bima nchini Tanzania.

Ujumbe huo umetoka Wizara ya fedha nchini Zimbabwe na taasisi mbalimbali za bima ikiwemo Insurance and Pensions Commission (IPEC), Insurance Council of Zimbabwe (ICZ) pamoja na Washauri wa Bima. Ziara hiyo inalenga kuwawezesha wageni hao kujifunza kuhusu uzoefu wa Tanzania katika maeneo ya bima ya afya kwa wote (Universal Health Insurance) pamoja na Bima ya Usafiri wa Baharini (marine insurance).

Katika ziara hiyo ya siku mbili, tarehe 24 na 25 Agosti 2026, ujumbe huo umepata fursa ya kufahamu kwa kina mifumo, mikakati na uzoefu wa Tanzania katika kusimamia na kuendeleza huduma za bima, hususan katika maeneo hayo mawili.

Kwa upande wa bima ya afya kwa wote, wageni hao wanatarajiwa kujifunza kuhusu namna Tanzania inavyotekeleza na kusimamia mifumo inayolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za bima ya afya kwa wananchi, pamoja na nafasi ya wadau mbalimbali katika kuhakikisha huduma hizo zinawafikia watu wengi zaidi.

Aidha, katika eneo la Bima ya usafiri wa baharini (marine insurance), ujumbe huo umepata fursa ya kujifunza kuhusu usimamizi wa bima zinazohusiana na shughuli za usafirishaji na biashara za majini, ikiwemo mifumo ya udhibiti, ufuatiliaji wa shughuli za bima na namna sekta hiyo inavyosaidia kulinda maslahi ya wafanyabiashara na wadau wanaojihusisha na shughuli za usafirishaji majini.

Ziara hiyo pia inatoa fursa kwa TIRA na taasisi hizo za Zimbabwe kubadilishana uzoefu kuhusu changamoto, mafanikio na mbinu bora katika usimamizi wa sekta ya bima. Mabadilishano hayo yanatarajiwa kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kuwezesha taasisi hizo kujifunza kutoka katika uzoefu wa kila nchi.

Kwa ujumla, ziara hiyo inaonesha umuhimu wa ushirikiano na kubadilishana maarifa miongoni mwa mamlaka na taasisi za bima barani Afrika, kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa sekta, kuongeza ufanisi wa huduma za bima na kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

TIRA, Kwa Soko Salama la Bima