Kampuni za Bima zatakiwa kushiriki utekelezaji wa Dira 2050
Kampuni za bima nchini zimetakiwa kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanapata elimu na kutumia huduma pamoja na bidhaa za bima kwa ajili ya kuboresha maisha yao.
Aidha, kampuni hizo zimetakiwa kuongeza uwekezaji katika sekta ya bima ili kuimarisha mchango wa sekta hiyo katika kukuza uchumi na kuongeza pato la Taifa.
Maelekezo hayo yametolewa na Kamishna wa mamlaka ya usimamizi wa Bima Tanzania,Dkt Baghayo Saqware, wakati akiendelea na ziara ya kikazi ya kutembelea kampuni za bima nchini, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhamasisha ushirikiano katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Katika ziara hiyo, Kamishna Saqware ametembelea kampuni ya Reliance Insurance, iliyopo Kinondoni, jijini Dar es Salaam, ambapo alizungumza na viongozi na watendaji wa kampuni hiyo kuhusu nafasi ya sekta ya bima katika kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa.
Akizungumza kwa niaba ya Reliance Insurance, Mkurugenzi Mkuu wa Fedha wa kampuni hiyo, Flora Makule, amesema kampuni hiyo inaunga mkono juhudi za sekta ya bima katika utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050, hususan kwa kuongeza uelewa wa huduma na bidhaa za bima kwa wananchi ambao bado hawajafikiwa na elimu hiyo.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Bodi ya Wakurugenzi wa Reliance Insurance, Shahid The Nai, amesema ziara hiyo imekuwa chachu ya kujadili kwa pamoja changamoto, mafanikio na fursa zilizopo katika sekta ya bima nchini.
Amesisitiza kuwa ushirikiano miongoni mwa wadau wa sekta ya bima ni muhimu katika kufikia malengo ya kitaifa, ikiwamo kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa bima na kupanua wigo wa matumizi ya huduma hizo.
Sekta ya bima inatarajiwa kuwa miongoni mwa sekta muhimu katika kufanikisha Dira ya Taifa 2050 kupitia kuongeza ulinzi wa kifedha kwa wananchi, kuchochea uwekezaji na kuchangia ukuaji endelevu wa uchumi.
