Kamishna wa Bima asisitiza ubunifu wa bidhaa kampuni za bima nchini
Kamishna wa Bima nchini Tanzania, Dkt. Baghayo Saqware, ameitaka Metro Life Assurance kuendelea kuboresha mipango na huduma zake, hususan katika ubunifu na uanzishaji wa bidhaa mpya za bima, ili kuongeza fursa za ajira na kuwafikia watumiaji wengi zaidi.
Dkt. Saqware ametoa rai hiyo wakati wa ziara yake ya kimkakati katika kampuni za bima nchini, ambapo ameielekeza Metro Life Assurance kuhakikisha inaweka mikakati madhubuti ya kuongeza faida na kujiimarisha katika ushindani wa soko la bima.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa kampuni hiyo kushughulikia madai ya wateja kwa wakati, kulinda maslahi yao na kutoa elimu ya kutosha kuhusu huduma za bima ili kuongeza uelewa na imani ya wananchi katika sekta hiyo.
Miongoni mwa maeneo mengine yaliyosisitizwa ni umuhimu wa kampuni kuongeza juhudi za kurejesha kwa jamii kupitia mipango ya Uwajibikaji kwa Jamii (Corporate Social Responsibility – CSR), pamoja na kupanua wigo wa upatikanaji wa huduma kwa kufungua matawi au vituo vya huduma katika maeneo mbalimbali nchini.
Hatua hiyo inalenga kuhakikisha wananchi wanapata huduma za bima kwa urahisi zaidi, hususan katika maeneo ambayo bado hayajafikiwa kikamilifu na huduma hizo.
Ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) kuendelea kushirikiana na kampuni za bima nchini katika kutathmini utendaji wa sekta, kubaini changamoto na fursa zilizopo, pamoja na kuweka mikakati ya pamoja ya kuimarisha sekta ya bima. Lengo ni kuhakikisha sekta ya bima inatoa mchango mkubwa zaidi katika maendeleo ya Taifa na utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050.
TIRA – Kwa Soko Salama la Bima.
