Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania

TIRA Logo
TIRA yasisitiza Ubunifu na Teknolojia Kuongeza Huduma za Bima kwa Wananchi
13 May, 2026
TIRA yasisitiza Ubunifu na Teknolojia Kuongeza Huduma za Bima kwa Wananchi

Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imewataka wadau wa sekta hiyo kuimarisha ubunifu na matumizi ya teknolojia ili kuongeza upatikanaji wa huduma za bima kwa wananchi. Wito huo umetolewa na Kamishna wa Bima Dkt. Baghayo A. Saqware wakati akifungua warsha ya Tanzania R3Lab kuhusu masuala ya ubunifu katika bima inayofanyika leo tarehe 13 hadi 14 Mei 2026 Southern Sun Hoteli, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika warsha hiyo, Kamishna amesema kuwa ubunifu si jambo la hiari tena katika sekta ya bima bali ni hitaji muhimu kutokana na mabadiliko ya teknolojia na matarajio ya wateja duniani. Ameeleza kuwa wananchi wanahitaji huduma za bima zilizo nafuu, rahisi kupatikana, zenye uwazi na zinazokidhi mahitaji yao. Aidha, ameipongeza FSD Africa na Cenfri kwa kushirikiana na TIRA katika kuandaa warsha hiyo.

Vilevile, amebainisha kuwa kiwango cha matumizi ya bima katika nchi nyingi za Afrika ikiwemo Tanzania bado ni cha chini, huku akisema kuwa ubunifu unaweza kusaidia kuwafikia wananchi ambao hawajapata huduma za bima kwa urahisi wakiwemo wanawake, vijana, wakulima wadogo na wafanyabiashara wadogo na wa kati. Ameongeza kuwa bado kuna changamoto zinazokwamisha ubunifu ikiwemo ukosefu wa miundombinu ya ubunifu, ushirikiano mdogo kati ya kampuni za bima na watoa teknolojia pamoja na mapungufu ya mfumo wa udhibiti wa teknolojia mpya.

Kwa upande wake, TIRA imesisitiza dhamira yake ya kuweka mazingira rafiki ya kikanuni yatakayowezesha ubunifu huku yakilinda maslahi ya wateja na uthabiti wa soko la bima. Miongoni mwa maeneo yaliyojadiliwa ni pamoja na kuanzishwa kwa mfumo wa “Regulatory Sandbox” kwa sekta ya bima nchini ili kusaidia majaribio ya ubunifu mpya kwa usalama. Kamishna wa Bima ametoa rai kwa washiriki kushiriki kikamilifu kwa kutoa mawazo na mapendekezo yatakayosaidia kujenga sekta ya bima ya kisasa, jumuishi na inayotumia teknolojia.

TIRA KWA SOKO SALAMA LA BIMA